GuidePedia

0
RAIS Jakaya Kikwete amemwapisha rasmi Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Juma Assad. Ameapishwa baada ya aliyekuwepo, Ludovick Utouh, kustaafu kwa mujibu wa Sheria na Katiba.
Mara baada ya kuapishwa CAG huyo alikabidhiwa ofisi pamoja na ripoti yenye kurasa 78 za mwongozo mzima kuhusu utendaji na changamoto za ofisi hiyo ya Ukaguzi. Utouh ndiye aliyemkabidhi.

Sherehe za kumwapisha kiongozi huyo, zilizofanyika Ikulu Dar es Salaam jana, zilihudhuriwa na viongozi wa Serikali, Kamati za Kudumu za Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) na Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na vyombo vya ulinzi na usalama.

Akizungumza mara baada ya kuapishwa Profesa Assad alisema atahakikisha anatekeleza ipasavyo na kwa uaminifu majukumu ya ofisi yake kwa kushirikiana na wenzake huku lengo kubwa likiwa ni kusimamia matumizi na mapato ya Serikali.

“Nitatekeleza kwa uaminifu majukumu yangu yote ya ofisi ya CAG kama yalivyoainishwa kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu,” alisisitiza.

Akijibu swali la waandishi wa habari kuhusu utata uliojitokeza kwenye ripoti ya CAG katika sakata la akaunti ya Tegeta Escow, hasa eneo ambalo ripoti hiyo imebainisha kuwa inawezekana fedha hizo ni za umma au la, alisema kwa sasa hawezi kuzungumzia suala hilo hadi atakapokabidhiwa ripoti hiyo na kuisoma.

Kwa upande wake, Spika wa Bunge, Anne Makinda, alisema uteuzi huo umekuja wakati mwafaka kutokana na ukweli kuwa kwa sasa nchi ipo katika kipindi cha mpito baada ya sakata la Escrow, hivyo ni wakati mwafaka wa kutengeneza sura halisi ya nchi yenye uwajibikaji na nidhamu ya fedha ya umma.

Alisema kutokana na hali ilivyo ni vyema Ofisi ya CAG na Bunge kwa pamoja, wakaunganisha nguvu ili kuhakikisha kunakuwa na uadilifu katika bajeti na matumizi ya fedha za Serikali.

“Kwa kweli mtikisiko huu ni mzuri katika uendeshaji wa nchi, unatufanya tukae sawa kwa kujenga nidhamu ya fedha, lakini pia utasaidia kujenga muundo mzuri wa kufanya kazi, ili nchi isimame vizuri ni lazima ipite kwenye hali iliyopo sasa,” alisema Makinda.

Waziri wa Fedha, Saada Salum Mkuya, alisema Wizara yake ina matarajio makubwa baada ya uteuzi huo wa CAG na itahakikisha inafanyakazi na ofisi hiyo kwa ushirikiano kwa manufaa ya Watanzania.

Akijibu swali kuhusu mwenendo wa maadili ya viongozi, hasa kutokana na sakata lililotikisa nchi la akaunti ya Escrow, Mkuya alisema wizara yake inaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuhakikisha taratibu, kanuni na sheria za fedha zinafuatwa.

“Maadili tunapambana nayo, wizara itahakikisha taratibu na sheria za fedha zinafuatwa, lakini pia tutaendelea kuwachukulia hatua wale wote wanaoenda kinyume na taratibu na sheria zilizopo, nawahakikishia suala hili tunalichukulia kwa mapana,” alisema.

Utouh alisema uteuzi huo umekuja wakati mwafaka kutokana na ukweli kuwa ofisi hiyo ni nyeti na si vizuri kukaa muda mrefu ikiwa haina CAG kamili, hali inayoweza kusababisha isiwe na nguvu.

Alisema tangu astaafu Septemba 19, mwaka huu, imepita miezi minne ofisi hiyo ikiongozwa na Kaimu CAG. “Nimewaachia ofisi iliyo madhubuti, imara na yenye wachapakazi, natumaini mazuri yote yataendelezwa kwa manufaa ya Taifa letu,” alisema.

Post a Comment

 
Top